dc.description.abstract | Tumeangazia Ubaguzi katika riwaya ya Mhanga Nafsi Yangu ya Said.A Mohamed. Tulichagua mada ya ubaguzi katika riwaya kwa sababu swala hili linatokea katika riwaya nzima ya Mhanga Nafsi yangu, na ni wajibu wetu kuwahamasisha Waafrika uhalisia wa mambo wanapohamia Peponi. Hii ni kwa sababu jamii zetu za Kiafrika zinahusudu Peponi kana kwamba hakuna shida zozote zipatikanazo huko na kuona kuwa watapata suluhu ya shida wanazokumbana nazo huko. Tulilenga vilevile kuchunguza changamoto zinazowakabili Waafrika Peponi na kuwazuia katika juhudi zao za kujikomboa kutoka katika matatizo mengi kama vile umasikini. Aidha ubinafsi, dhuluma, utabaka uliokithiri na ubaguzi ni baadhi tu ya changamoto wanazokumbana nazo Waafrika Peponi.Utafiti wetu umeongozwa na nadharia ya Uhalisiajabu tukijikita katika kiunzi chake kinachodai kuwa Uhalisiajabu hueleza kadhia zinazotendeka katika maisha ya mtu ambapo uhalisi na ndoto, kifo na uhai, usasa na uzamani, shamba na mjini, ugeni na wenyeji huingiliana kiasi kwamba mpaka uliopo baina ya hali hizi ni mdogo sana. Mwongozo huo umetufanya kuitathmini jamii mwanzo kabla ya kuutalii ubaguzi katika riwaya husika. Kutokana na utafiti wetu, imebainika kuwa Said.A Mohammed amefaulu katika kuisawiri jamii ya Waafrika inavyobaguliwa na jamii ya Wapeponi na asasi zinazoendeleza ubaguzi kama vile sheria, ndoa, polisi, na pia elimu Aidha mwandishi ametoa mchango wake muhimu katika kuwajenga wanaobaguliwa kihadhi. | en_US |