Usawazishaji Wa Leksimu Katika Kiswahili: Utafiti Kifani Wa Vihiga
Abstract
Utafiti huu unahusu usawazishaji wa leksimu katika Kiswahili kwa kujikita katika eneo la Vihiga lililoko Magharibi mwa Kenya. Utafiti huu unahusu aina za mabadiliko ya maana zinazohusika katika kuelezea maana za maneno katika Kiswahili. Nadharia ya Pragmatiki Leksika ndiyo iliyotuongoza kwa kiasi kikubwa katika utafiti huu. Nadharia hii imetusaidia katika kuchunguza dhana iliyosimbwa na neno kwenye tamko na michakato ya kiakili inayompitikia msikilizaji katika kufasiri dhana iliyosimbwa na neno ili kufikia uhusiano. Katika utafiti huu, tumetoa tatizo la utafiti, maswali ya utafiti, malengo ya utafiti na nadharia tete. Vilevile tumetoa muhtasari kuhusu kaunti ya Vihiga na soko la Mbale ambalo ni eneo la utafiti. Aidha, tumeelezea umuhimu wa kufanya utafiti huu, upeo na mipaka, udurusu wa yaliyoandikwa kuhusu mabadiliko ya kisemantiki na yaliyoandikwa kuhusu nadharia ya utafiti. Msingi wa nadharia ya utafiti umeelezwa kwa kina pamoja na mihimili muhimu ya nadharia hii. Tulitumia mbinu za kushiriki shughuli, mahojiano, majadiliano na kurekodi miitikio ya washiriki katika kukusanya data yetu katika eneo la Vihiga. Katika utafiti huu, tumeainisha na kuchanganua aina za mabadiliko ya maana zinazotokea katika Kiswahili kwa mujibu wa Nadharia ya Pragmatiki Leksika. Kuna aina mbili kuu za mabadiliko ya maana zinazotokea katika Kiswahili –ubanaji wa kileksika na upanuzi wa kileksika. Sababu za usawazishaji wa leksimu katika Kiswahili zimeelezwa. Ilidhihirika kwamba, sababu za mabadiliko ya maana zinazoibuka katika utafiti huu ni za kiisimu. Aidha, athari za usawazishaji wa maana zimetathminiwa. Maneno ya Kiswahili yanapata athari mbili kuu za mabadiliko ya maana ambazo ni, badiliko katika mawanda na badiliko katika tathmini. Badiliko katika mawanda linajumuisha kupanuka na kubanika kwa maana. Badiliko katika tathmini linajumuisha msawajikomaana na uemeshajimaana. Yapo maneno ambayo yanapata athari zaidi ya moja kama vile kupanuka maana na kubanika maana mtawalia au msawajikomaana na uemeshajimaana mtawalia. Mwisho, matokeo ya utafiti huu yametathminiwa na nadharia tete zote kushikiliwa. Aina mbalimbali za mabadiliko ya maana zinazotokea katika Kiswahili zilibainika na ziliweza kuelezwa kwa misingi ya Nadharia ya Pragmatiki Leksika. Sababu za mabadiliko ya maana katika leksimu za Kiswahili zilikuwa za kiisimu na ziliibuka kutokana na miktadha ya matumizi ya maneno hayo. Matokeo ya utafiti yamebainisha kwamba, kuna kudhoofika au kupotea kwa mawasiliano katika Kiswahili kwa sababu ya mabadiliko ya maana za maneno yanayoathiri miktadha iliyozoeleka.
Publisher
University of Nairobi
Rights
Attribution-NonCommercial-NoDerivs 3.0 United StatesUsage Rights
http://creativecommons.org/licenses/by-nc-nd/3.0/us/Collections
The following license files are associated with this item: