dc.description.abstract | Utafiti huu ulichunguza jinsi sitiari za Kiswahili hujitokeza katika kauli za wanasiasa na jinsi
wanasiasa huweza kuzitumia kueneza kauli za kichochezi nchini Kenya. Vile vile, jinsi lugha ya
Kiswahili ijapokuwa ni lugha rasmi na ya kitaifa inayotakikana kuunganisha wananchi
huchangia kueneza kauli za kichochezi katika siasa nchini Kenya, jinsi lugha ya Kiswahili
huweza kutumiwa kama chombo cha kuleta uwiano wa kijamii nchini Kenya. Lengo kuu la
utafiti huu lilikuwa kuchambua matumizi ya sitiari za Kiswahili katika kauli ya kichochezi
kwenye diskosi ya kisiasa nchini ili kubaini na kuchunguza michango yao katika kueneza kauli
za kichochezi katika siasa za Kenya. Utafiti huu ulinuia kuchangia pakubwa katika tafiti
zilizopo, na kuongeza maarifa mapya katika pengo la kiusomi katika eneo la mchango wa sitiari
za Kiswahili katika kauli za kichochezi kwenye diskosi ya kisiasa nchini Kenya. Njia ya utafiti
ya mtandao wa Youtube, maktabani na data kutoka kwa tume ya Kitaifa ya Uwiano na
Utangamano (NCIC) ilitumika kuleta maelezo ya mada chini ya uchunguzi kwa kutumia
nadharia ya vitendo usemi. Data ilichambuliwa kwa kuzihusisha na malengo ya utafiti. Utafiti
huu umebaini kuwa, sitiari ina mchango mkubwa katika semi zozote, inachangia pakubwa katika
kueneza kauli ya chuki katika siasa nchini Kenya kwa kuwagawanya na kuwadunisha jamii
lengwa. Wanasiasa mara nyingi hutumia sitiari kwenye matamshi yao kwenye kampeni kwa njia
ya kushawishi wafuasi wao na pia kuwachochea dhidi ya jamii pinzani. Lugha ya Kiswahili
ijapokuwa ni lugha ya taifa na rasmi nchini Kenya ina mchango katika kueneza kauli ya chuki
siasani kwa kutumia msamiati ambao wanasiasa hutumia kama matusi dhidi ya jamii nyingine.
Vile vile, lugha ya Kiswahili inaweza kutumika kuleta uwiano wa kijamii nchini Kenya. Hata
hivyo, licha ya kubuniwa kwa sheria na sera za kukabili hotuba na matamshi ya chuki nchini
Kenya, bado kuna changamoto zinazozuia makabiliano dhidi ya kauli ya chuki katika siasa. | en_US |