dc.description.abstract | Katika kazi hii tumechanganua kiisimu baadhi ya matini za fasihi ya Kiswahili kwa mtazamo wa Pragmatiki Leksika. Tumeigawa kazi hii katika sura tano. Sura ya kwanza imeshughulikia utangulizi wa kijumla kuhusu mada, usuli wa mada, tatizo la utafiti, madhumuni ya utafiti, nadharia tete, sababu za kuchagua mada hii, upeo na mipaka ya utafiti huu, msingi wa nadharia, njia za utafiti, ukusanyaji na uchanganuzi wa data na umuhimu wa utafiti huu. Sura ya pili imechunguza ukuaji wa riwaya ya Kiswahili, baadhi ya migao ya misamiati inayopatikana katika baadhi ya lugha kama vile Kiswahili, hali ambazo husababisha kupanuka kwa msamiati wa lugha fulani, historia ya mwandishi wa Kiza Katika Nuru, baadhi ya mbinu za uandishi na mwisho tumejadili mtagusano kati ya isimu na fasihi.
Sura ya tatu imeshughulikia uchanganuzi wa data ambao umeegemezwa kwenye kategoria za matukio ya kimsingi zilizofafanuliwa na Wilson (2003) na Carston (2002) ambazo zinahusu kubanika kwa maana, kisio la maana na kupanuka kwa maana. Sura ya nne inahusu tathmini ya baadhi ya matumizi ya semi na misamiati katika matini ambazo tumezichanganua. Sura ya tano inahusu muhtasari, hitimisho la kazi nzima na mapendekezo ya masuala ambayo yanaweza kushughulikiwa katika tafiti zitakazofanywa katika siku za usoni.
Lengo la utafiti huu lilikuwa kutathmini nadharia tete kwamba: Nadharia ya Pragmatiki Leksika inaweza kutumika kuchanganua vizuri matiniza Kiswahili, semi katika matini za Kiswahili huzua maana ambazo ni pana katika misingi ya Pragmatiki Leksika na pia uhusiano wa usemi na muktadha ni muhimu katika kufasiri maana kwa misingi ya Pragmatiki Leksika. Matokeo vanaonyesha kuwa nadharia tete zote zimeafikiwa. | en_US |