dc.description.abstract | Utafiti huu ulichunguza jinsi wazungumzaji hutumia misimbo inayozua uwazi na
umaanisho katika lugha za Kiswahili na Ekegusii kwa lengo la kubainisha kama
kuna mlingano wowote kati ya lugha hizi, zote zikiwa lugha za Kibantu. Lugha
hizo zimeelezwa kisemantiki ambapo maana msingi za kauli zimechanganuliwa,
na baadaye maana za kipragmatiki kuelezwa kwa kutumia Nadharia ya Uhusiano.
Nadharia ya Uhusiano ya Sperber na Wilson (1986) ilitumiwa kufasiri misimbo
iliyotokana na kategoria mbalimbali za lugha hizi mbili ambapo kanuni za
uhusiano pamoja na kanuni ya ujuzi wa msikilizaji zilisaidia kupata fasiri
iliyokusudiwa na wasemaji wa kauli mbalimbali.
Tasnifu hii ina sura nne. Katika sura ya kwanza, tumeshughulikia utangulizi kwa
jumla. Tumeeleza kuhusu lugha za Kiswahili na Ekegusii, tatizo la utafiti,
madhumuni ya utafiti, nadharia tete, sababu za kuchangua mada, upeo na mipaka
misingi ya nadharia, yaliyoandikwa kuhusu mada yetu pamoja na mbinu za utafiti
tulizotumia.
Katika sura ya pili, tumejadili kuhusu kategoria za kisemantiki kwa jumla ambapo
tumebainisha makundi mawili makuu ya kisemantiki ambayo ni pamoja na
kategoria za kileksika na kategoria za kimuktadha.
Sura ya tatu imejadili kategoria mbalimbali za kisemanti ambazo huibuka
kimazungumzo katika lugha ya Kiswahili na vilevile lugha ya Ekegusii na kueleza
uwazi na umaanisho wa kauli hizo. Ufafanuzi wa maana kiumaanisho umefanywa
kwa kutumia mbinu za kinadharia za uhusiano. Nadharia ya Uhusiano ilitumiwa
ambapo ilibainika kwamba lugha hizi mbili zinatumia mitindo tofauti kuzua
umaanisho. Aidha, tofauti za kiuteuzi wa maneno zimebainishwa katika lugha
zote. Sababu za tofauti hizo zimejadiliwa.
Katika sura ya nne, mahitimisho na mapendekezo yametolewa ambazo nadharia
tete pamoja na madhumuni ya utafiti yametathminiwa. Kutokana na tathmini hizo
pamoja na uchanganizi wa data yetu, tumerejelea nadharia tete zetu ambapo
baadhi zimekubaliwa na nyingine kukanushwa. Vilevile, katika sura hii tumetoa
mapendekezo ya tafiti za baadaye.
Uchanganuzi wa misimbo mbalimbali ulidhihirisha tofauti za uteuzi wa kategoria
za kisemantiki zinazotumika katika lugha za Kiswahili na Ekegusii, na maana
zilizosimbwa pia zilibainisha tofauti kadha wa kadha. Hali hii ilibainishwa na
tofauti za fahamu za awali za tamaduni katika lugha hizo mbili, mitazamo pamoja
na mazingira ya watumizi wa lugha hizi. | en |