Umenke na ubaguzi wa kijinsia katika methali na vitendawili vya Kiswahili
Abstract
Utafiti huu unahusu umenke na ubaguzi wa kijinsia dhidi ya wanawake na jinsi unavyojitikeza katika methali na vitendawili vya Kiswahili. Kila siku tunasoma vitabu vingi vya riwaya,tamthilia na mashairi yanayozungumzia ubaguzi wa wanawake na juhudi za ukombozi wao. Hata hivyo ni nadra kukutana na chambuzi za maumbo kama methali na vitendawili vinavyohusu ubaguzi wa kijinsia, kwa kufafanua waziwazi na kutolea mifaao maradufu.
Katika utafiti huu tulidhamiria kujaza pengo hili ilmradi kazi za namna hii ziongezeke. Aidha utafiti huu ulidhamiria kuchunguza kwa kina na kwa waziwazi yaliyofichama katika methali na vitendawili vya kiswahili kuhusu jenda na ubaguzi wa kijinsia.kwa hivyo, tatizo lililotushughulisha katika kazi hii ni methali na vitendawili vinavyokosa kuwasawazisha watu kijinsia katika matumizi yake.
Madhumuni yetu yalikuwa kuchunguza na kuweka wazi miundo-msingi ya kijamii na mbinu zinazotumiwa na methali na vitendawili na kuishia kubagua watu (has a wanawake) kijinsia. Kimsingi tulitumia vitabu viwili: Kamusi ya Vitendawili, Tashbihi na Mishangao (Wamitila, K.W 2004) na Kamusi Changanuzi ya Methali (Waihiga, G. na Francis K. 2007). Mifano zaidi imetolewa kutoka vitabu mbalimbali vya kifasihi.
Sehemu kubwa ya utafiti huu ilijikita katika usomaji maktab ani , kusoma makala, vitabu na tasnifu mbalimbali. Pia, kwa kiasi kidogo, tulitumia tovuti kuhusu jamii ya Waswahili, suala la umenke na nadharia ya ufeministi. Matokeo ya utafiti yalidhihirisha uwepo ubaguzi wa kijinsia dhidi ya wanawake kwa kiasi kikubwa na dhidi ya wanaume kwa kiasi kidogo sana. Nadharia ya ufeministi tuliyotumia ilitupa mwongozo mwema katika kutambua haya.
Tunatumai kuwa utafiti huu utakuwa wa manufaa kwa wasomi na watafiti wanaovutiwa na uchunguzi wa ubaguzi kijinsia.
Publisher
University of Nairobi, Kenya